Beruflich Dokumente
Kultur Dokumente
Ukaribisho
Nianze kwa kuwakaribisha nyote kwenye Semina Elekezi inayojumuisha Mawaziri, Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu na
Naibu Makatibu Wakuu. Kama lilivyo jina lake, Semina hii ni ya kuelekezana juu ya namna tutakavyotimiza majukumu yetu
katika Serikali. Tulikuwa na Semina kama hii mwaka 2006. Imetusaidia kupata mafanikio tuliyoyapata miaka mitano
iliyopita. Naamini na Semina hii itatusaidia kupata ufanisi tunaoutarajia na ambao wananchi wanautarajia kutoka kwetu.
Madhumuni ya Semina
Ndugu Viongozi,
Katika Semina hii majukumu ya msingi ya Serikali ya utawala, maendeleo na ulinzi na usalama yatafafanuliwa. Pia itaelezwa
jinsi kila mmoja wetu anavyohusika nayo na anavyotegemewa kutimiza wajibu wake. Katika hotuba yangu ya kuzindua
Bunge nilitaja malengo 13 ambayo yamejumuisha mambo makuu tutakayoyapa kipaumbele katika Serikali katika miaka
mitano hii. Lakini nilikumbusha kuwa yale mambo 13 ni muhtasari wa maelekezo yaliyomo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya
Chama cha Mapinduzi.
Ndugu Mawaziri;
Mtakumbuka kuwa katika mkutano wangu wa kwanza nanyi niliwasisitizia umuhimu wa Ilani ya Uchaguzi kwa kila mmoja
wenu na kwa Serikali yetu kwa jumla. Niliwaambia kuwa Ilani ndiyo mkataba mkuu baina ya Chama cha Mapinduzi na
wananchi. Utekelezaji wake ndicho kipimo kikuu cha uwezo wetu wa kuongoza, mwaka 2015. Niliwataka kila mmoja wenu
atambue ukweli huo na kutengeneza mkakati wa kutekekeleza Ilani kwa yale mambo yanayohusu Wizara yake. Sina shaka
kuwa takriban miezi mitano baadae kila mmoja wetu atakuwa amekamilisha kazi hiyo na kuingiza katika mipango ya kazi ya
Wizara itakayotekelezwa kuanzia bajeti itakayowasilishwa Bungeni mwezi ujao.
Ndugu Mawaziri na Ndugu Makatibu Wakuu;
Siku ile pia nilisisitiza jambo kwa Mawaziri ambalo napenda kulirudia tena leo kwani linawahusu na Makatibu Wakuu. Ninyi
kwa pamoja, Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu ndiyo timu moja ya uongozi na utawala katika
Wizara. Kama viongozi mnategemewa kuonyesha njia kuhusu nini cha kufanya kutekeleza majukumu ya Wizara
nilizowakabidhi kuziongoza.
Katika jukumu lenu la utawala mnategemewa kuwa makini na mahiri katika kutumia rasilimali watu, vifaa na fedha za umma
mlizokabidhiwa katika kutekeleza majukumu yenu. Mnategemewa kuwa na mipango na mikakati thabiti ya kutekeleza
majukumu hayo.
Kuisemea Serikali
Ndugu Mawaziri na Ndugu Makatibu Wakuu;
Moja ya mada ya semina hii inahusu mawasiliano ya Serikali. Kwa maneno mengine kuisemea Serikali. Hili ni jambo
ambalo tuna udhaifu mkubwa. Sijui kwanini hatuwi wepesi kuyasemea mafanikio mengi tuliyoyapata tukaacha wasiotutakia
heri wanaosema hatukufanya kitu wasikike mpaka waonekane wanasema kweli. Mwanazuoni mmoja bingwa wa habari
aliwahi kusema kuwa “kufanya kitu bila kuufahamisha umma ni sawa kama kitu hicho hakijafanyika.” Mwingine anasema
kuwa uongo ukisemwa mara nyingi hugeuka kuwa ukweli.
Uzoefu wa miaka mitano umeonyesha kwamba tumefanya mambo mengi lakini wananchi hawakuelezwa ipasavyo. Pia,
tumeacha upotoshaji kufanywa bila ya kusahihishwa au kuchelewa sana kusahihishwa. Hivyo basi, wananchi wamekuwa
wakijikuta wakiamini uongo na kulaumu au hata kuichukia Serikali kwa mambo ambayo ni potofu. Wangeambiwa ukweli
mapema hawangefikia hapo. Lazima upungufu huo tuondokane nao. Lazima tuwe makini na hodari kuelezea shughuli
zinazofanywa na Serikali, mafanikio yanayopatikana na changamoto zilizopo.
Aidha, tuwe wapesi kusahihisha upotoshaji wowote unaofanywa dhidi ya Serikali. Kutokufanya hivyo kumetugharimu sana.
Hatuwezi kuendelea hivi wakati ninyi viongozi mpo, watu Mawizarani wapo, rasilimali zipo na vyombo vya habari vipo
vinasubiri kupewa habari.
Ndugu Viongozi;
Hakika tumefanya mengi na mafanikio yanaonekana, lakini tunayo kazi kubwa sana mbele yetu ya kufanya. Tanzania ni
miongoni mwa nchi 49 maskini sana duniani. Shabaha yetu kubwa ni kutoka hapa tulipo sasa na kuwa nchi ya uchumi wa
kati ifikapo mwaka 2025. Yaani, tutoke kwenye pato la wastani la USD600 la sasa hadi pato la USD1,500 mpaka USD3,000
mwaka huo.
Niliamua na kuelekeza kuwa yafanyike mapitio ya Vision 2025 na tuigawe miaka 15 iliyosalia katika mafungu matatu ya
miaka mitano mitano. Tuwe na mipango ya maendeleo ya miaka mitatu tukianzia na huu unaowiana na kipindi chetu cha
uongozi. Hii itatuongoza vizuri zaidi kuelekea na kufikia lengo. Kazi ya mapitio inaendelea kama ilivyo ile ya matayarisho
ya mpango wa kwanza wa maendeleo. Katika Semina hii tutapata maelezo ya awali ya kazi inayoendelea.
Ndugu Viongozi na Ndugu Washiriki;
Tunao pia Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini (MKUKUTA) ambao tumekuwa tunautekeleza tangu mwaka
2005. Tumekamilisha MKUKUTA I na hivi sasa tupo kwenye utekelezaji wa MKUKUTA II ambao utakamilika mwaka 2015.
MKUKUTA umetusaidia sana katika kuainisha maeneo ya kipaumbele katika bajeti. Kwa ajili hiyo, imesaidia katika jitihada
za Serikali za kupunguza umaskini na kuinua hali ya maisha ya Watanzania. Bila ya shaka tutapata nafasi ya kuelezwa
maudhui ya MKUKUTA II ili tuelewe namna ya kuwianisha shabaha zake na shughuli tunazozifanya katika Wizara zetu.
Ulinzi na Usalama
Ndugu Mawaziri na Ndugu Makatibu Wakuu;
Katika semina hii tutapata nafasi ya kuzungumzia masuala ya ulinzi na usalama. Tutawasikiliza Wakuu wa Vyombo vya
Ulinzi na Usalama kuhusu usalama wa nchi. Pia tutamsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU kuhusu mapambano dhidi
ya rushwa na Kamishna wa Tume ya Maadili ya Viongozi kuhusu uadilifu wa viongozi.
Hitimisho
Ndugu Viongozi Wenzangu,
Ni matumaini yangu kwamba maneno haya ya utangulizi niliyosema, yatatupatia msingi wa tafakuri katika mijadala na
mafunzo tutakayopatiwa katika siku nne zijazo hasa katika maeneo makuu ya semina ambayo ni pamoja na mfumo wa
utawala na utendaji; uchumi na maendeleo; utawala bora; ulinzi na usalama; muungano; na masuala mtambuka.
Nimeambiwa kwamba semina hii itaendeshwa kwa utaratibu wa mihadhara kwa ajili ya kuwasilisha mada pamoja na
majadiliano ya pamoja. Pia nimearifiwa kuwa kutakuwepo majadiliano katika vikundi ili kuchambua kwa undani zaidi mada
zilizowasilishwa. Hivyo, rai yangu kwenu nyote muwe tayari kushiriki kwa ukamilifu katika majadiliano kwenye mihadhara
kwa ukweli na uwazi bila kujali tofauti ya nyadhifa zenu. Wote muwe huru kutoa maoni yenu. Ndiyo maana tuko hapa.
Ndugu Viongozi,
Nawashukuru watoa mada waliokubali kuchangia ujuzi na uzoefu wao nasi. Baada ya kusema hayo sasa napenda kutamka
kwamba Semina Elekezi kwa Viongozi na Watendaji Wakuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imefunguliwa
rasmi.